KWAHERI DADANGU CHANYA

Posted in Poems

KWAHERI DADANGU CHANYA

KWAHERI DADANGU CHANYA

in Poems By Dcf on 21 Jun 2018

Naanza kwa jina lake, mtukufu maulana
Atupe rehema zake, atuongoze bayana
Kila mtu ana yake, sikuye hawezi kana
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Umeyatenda ni mengi, Agnesi hadi Loreto
Chuoni pia kwa wingi, bila laiti majuto
‘Katupa furaha nyingi, yenye sifa ya uzito
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Tabasamu yako tamu, kila mara hadi sasa
Kicheko ja kilaamu, chenye sifa ya kisasa
Maneno tamu hamamu, hekima bila siasa
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Twakukumbukia wema, ulotenda ni kathiri
Na mengi uliyosema, hatuwachi kukariri
Mola akulaze pema, peponi akusitiri
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Mswiba umetuswibu, umetuacha swahibu
Tulimpenda ajabu, halingani na dhahabu
Hatuna katu majibu, kwa kifo kilikuswibu
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Ni pigo kwetu chuoni, hata chuoni Loreto
‘Metuacha huzuni, na maisha ya majuto
Tulikuenzi mwandani, kipenzi chetu cha uto
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Rambirambi nyingi sana, ziwafikie nyumbani
Farajaze maulana, kwa ndugu na majirani
Inshallah tutamwona, kipenzi chetu peponi
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

Rabana yetu sikia, waja tunakulilia
Sisi kwako tunajua, ni lazima kurejea
Tuelekeze hatua, tusije potea njia
Kwaheri dadangu Chanya, pema mola akulaze

©Silah Moh’d
All rights reserved
©2017

Dcf

Author : Dcf

The Daystar Christian Fellowship (DCF) is the umbrella body for all student-led ministry activities and fellowship. These ministry activities provide opportunities for life and spiritual growth through discovery of gifts and talents and providing opportunities to utilize them.

Read Also Related Posts

Want to join? Leave a Comment